KWELI ELIMU HAINA MWISHO, HEBU KUTANA NA BIBI MWENYE MIAKA 90 AMBAYE ANASOMA SHULE YA MSINGI




Kuna ule usemi usemao elimu haina mwisho, na kauli hiyo inadhibitika vizuri nchini Kenya baada ya mwanamke mwenye umri wa miaka 90 nchini humo kuhudhuria masomo na hivyo kuifanya dunia kuamini kuwa huenda mwanamke huyo ndiye mwanafunzi mzee zaidi nayesoma shule ya msingi duniani.


Bibi huyo ambaye anaitwa Prissilla Gogo Sitienei akiwa na wajukuu zake wapatao sita alijiunga na shule ya 'Leaders Vision Preparatory School' miaka mitano iliyopita, hivyo kwa sasa yupo darasa la tano, lakini pia inaelezwa aliwahi kuwahudumia wakaazi wa kijiji chake cha Ndalat kilichoko kwenye bonde la ufa kama mkunga miaka sitini na mitano iliyopita.

Priscilla anapokuwa darasani huketi dawati la mbele kabisa, huku akiwa amevalia nguo zake za shule na inaelezwa kwamba amekuwa ni msikilizaji mzuri wa walimu wanapofundisha, lakini pia amekuwa ni msaada mkubwa kwa wanafunzi wengine ambao wana umri kati ya miaka 10 hadi 14 na mara zote amekuwa akiwapa ujumbe wanafunzi wengine hasa mabinti na kuwaambia kuwa elimu ndiyo urithi wao.
Priscilla Gogo Sitienei akiwa darasani na wanafunzi wenzake.


Aidha, Priscilla anajulikana zaidi kama Gogo maana yake ikiwa ni bibi katika lugha ya jamii ya wakalenjini, anasema anafurahia masomo akiwa na umri wa miaka 90 katika umri huo anajua kuandika na kusoma pia ni fursa aliyoikosa alipokuwa mdogo.

Hata hivyo, Priscilla hujihisi huru zaidi anapotumia lugha mama yaani ki Kalenjin kuliko kiingereza, lakini pale anapoulizwa ni kwanini aliamua kujiunga na shule katika umri wake huo mara zote husema kwamba  aliamua hivyo ili aweze kumudu kusoma bibilia, lakini pia kwa umri wake anataka awahamasishe watoto kupata elimu, kwani anawaona watoto wengi wakiwa hawako shuleni na watoto hao wana watoto.

Hata hivyo, inaelezwa kuwa Gogo amekuwa ni balozi mzuri wa mambo ya elimu kwani kila apitapo mitaani huwa haoni shida kukabiliana na watoto ambao hawako shuleni katika muda wa masomo na kuwauliza kwanini hawako shuleni.

Gogo anasema watoto hao humjibu kwamba hawaendi shule kwakuwa umri wao ni mkubwa, lakini yeye huwaambia “mimi ni mkubwa sana kwenu, lakini niko shuleni hivyo nanyi jiungeni na shule.”

Sambamba na hayo, kikubwa kinachomuumiza Gogo ni pale anapowaona watoto wengi waliopoteza muelekeo, huku wengi wao wakiwa hawana baba na wanazurura hovyo mitaani, bila msaada wowote na anasema kutokana na hali hiyo anataka kuwahamasisha waende shuleni.

Chanzo : BBC Swahili

No comments:

Post a Comment

Ad Inside Post

Comments system

Disqus Shortname